Saturday, February 28, 2009

NGOJA LEO TUANGALIE:- MWANAUME NA MWANAMKE MAHITAJI YAO.

Katika maisha yetu ya kila siku, mara nyingi twasikia:- ”nahitaji nguo mpya” au ”nahitaji kutengeneza paa la nyumba yangu”. Au, “Nahitaji fedha”; “Nahitaji chakula”. Neno “hitaji” twalitumia hata katika mambo mengi. Baada ya kuumwa na mbu nahitaji kujikuna ili kupunguza kuwasha. Au ninapokuwa na hofu najisikia kama nahitaji mtu wa kunisaidia.

Aina mbalimbali za mahitaji:-
Sisi wanadamu tuna mahitaji ya aina nyingi. Mengine siyo makubwa. Mara mahitaji hayo yatimizwapo, tunapata furaha kwa muda mfupi na kuonekana tumetosheka. Mahitaji mengine ni muhimu na ya msingi katika maumbile yetu. Ni ya lazima kwa maisha yetu. Mahitaji haya tukiyapata, twasikia raha. Yasipotimizwa tunakuwa na udhaifu, huzuni na umaskini. Sio umaskini wa fedha bali wa afya, au ukosefu wa raha na amani.

Sasa tuone mahitaji yaliyo muhimu kwa sisi wanadamu wote. Mahitaji haya anayo kila mmoja – mwanamume na mwanamkw - ingawa kila mmoja anayadhihirisha kwa njia tofauti. Mahitaji haya yaweza kugawanyika katika sehemu tatu:- mahitaji ya kimwili, mahitaji ya kimoyo (hisi) na mahitaji ya kiroho.

Mahitaji ya Kimwili
Kwanza kabisa, kuna yale mahaitaji muhimu ya mwili:- kupumua hewa, kula, kunywa, kupumzika na mahali pa kukaa. Haya ni mambo muhimu na ni lazima mtu ayapate. Tunajua yanayompata mtu aliyekosa hewa. Ikiwa chembechembe za ubongo wake zinakosa hewa safi, anaweza kuanza kusikia kizunguzungu, baadaye kuzimia na kufa.

Tunajua pia kwamba ili tuishi ni lazima tule na tunywe. Ni watu wachache sana wawezao kustahimili njaa kwa muda wa siku 10. Usingizi na kupumzisha mwili ni jambo muhimu pia. Mwili wetu unahitaji kujenga nguvu mpya kwa njia ya mapumziko. Tunahitaji nguvu mpya kuendelea na shughuli zetu za kawaida.

Kati ya mahitaji haya ya mwili kuna lingine, nalo ni lile lililomo katika maumbile yetu, yaani katika utu ume au utu uke. Ndiyo haja ya kufanya mapenzi. Tunaelewa kwamba jambo hili ni la msingi katika maumbile yetu. Ni wazi kwamba haja hiyo hutaka kujidhihirisha. Mwanaume atafikiri kama mwanaume na atafanya kazi kama alivyo: atapenda kama mwanaume. Hali kadhalika mwanamke. Wakati mwingine hamu ya kumhitaji mwanaume au mwanamke inaonyeshwa katika tendo la kukaribiana; lakini hii si njia tu pekee ya kuonyesha mapenzi.
Mahitaji ya kiroho (Hisi)
Lipo kundi la pili la mahitaji tungeweza kuyaita mahitaji ya ndani, mahitaji ya moyoni. Mahitaji haya ni yale ya hisi. Watu waliojifunza elimu ya akili na moyo wa binadamu wanatambua kwamba kuna mambo manne ambayo kila mmoja wetu anahitaji:- Usalama – Kukubalika katika jumuiya – Kuthaminika – na Kujikamilisha binafsi: Tutaangalia kwa undani kila moja si muda mrefu:-
.

Friday, February 27, 2009

USAFIRI TANZANIA/DAR ES SALAAM

Muda mrefu imekuwa inasemekana kutakuwa na mabadiliko ya usafiri nchini Tanzania. Lakini mpaka leo hakuna kinachoonekana. Nina maana kwa sasa hasa jijini Dar es salaam kuna tatizo kubwa la usafiri yaani daladala ni nyingi mno kiasi kwamba ni fujo tu. Afadhali kutembea au kutumia baiskeli kwa jinsi foleni za daladala zinavyosongamana. Naweza nikasema hakuna maana kuwa na gari Dar, kwenda kazini inabidi ujihimu mapema sana na ukichelewa basi itakuwa ule mtindo wa foleni. Na ukitaka kwenda sehemu ni afadhali ujue ni muda gani mzuri sio kuondoka tu.

Sijui mwenzangu mnasemaje? Kwani binafsi ningependa au pendekeza daladala zote zitolewe na kuwe na mabasi makubwa na pia train ya haraka. Nadhani kungekuwa na nafuu sana kwa wananchi. Kwa sasa naweza nikasema kwa kweli ni fujo, fujo, fujo sana. Maana magari mengi sana, pikipiki nyingi mno na daladala ndo uchafu tu.

Thursday, February 26, 2009

NATAKA KUMSHUKURU MUNGU KUWA NIMESAFIRI SALAMA

Habari za siku chache wanablog na wasomaji wote napenda kuchukua nafasi hii na kusema ya kwamba, nimesafiri salama na nimerudi tena hapa kijiwe. Ili niweze kuwa nanyi pia napenda kuwashukuru woooote kwa sala na upendo wenu nakujua mlikuwa mnaniombe nisafiri salama. Ni hayo tu.